Sunday, December 20, 2009

Waridi.

Ua ninakutafuta, tayari ushachanua,
Marashi nanayapata,manukato yavutia,
Ni lini nitakupata,uzuri najivunia,
Waridi nakutafuta, nataka kujichumia.


Niite unionapo, wala usibabaike,
Sijui wapi ulipo,paza sauti iskike,
Ipi ni njia mkato, haraka mimi nifike,
Waridi nakutafuta, nataka kujichumia.


Ni mengi ninayaona, maua ya kupendeza,
Ni lipi lililonona,si kazi ya kubeza,
Waridi ndo lanikuna,ua litaniliwaza,
Waridi nakutafuta, nataka kujichumia.

Waridi ninakusaka,wa maisha jitokeze,
Mbali pia nitafika,ulipo wewe nijuze,
ua umeshapevuka,nakuchuma nikutunze,
Waridi nakutafuta, nataka kujichumia.

Bustanini ninapita,tayari kujichumia,
Tabia itanivuta,ua kufuatilia,
Najua nitalipata,maisha tafurahia.
Waridi nakutafuta, nataka kujichumia.

Friday, October 9, 2009

Maisha

Maisha kweli ni fumbo,lilogumu kufumbua,
Leo lakupiga kumbo,kesho wachekelea,
Punde yezaenda kombo,sharti kujikwamua,
Maisha ndivyo yalivyo,ya kesho huwezi jua.


Maisha yamesheheni,uzuri pia ubaya,
Ungalipo duniani,usiyaonee haya,
Popote yatafuteni,msichoke kusakanya,
Maisha ndivyo yalivyo,ya kesho huwezi jua.


Usitukane wakunga,na uzazi bado upo,
Mlango utafunga,ungali ndani haupo,
Meli maisha tasonga,taachwa hapo ulipo.
Maisha ndivyo yalivyo,ya kesho huwezi jua.


Njiani utayakuta,majabali vizingiti,
Huna budi kuyapita,viunzi havikwepeki,
Kamwe hakuna kujuta,maisha nasbu bahati,
Maisha ndivyo yalivyo,ya kesho huwezi jua.

Monday, September 21, 2009

Majuto

Mtegoni nimekwama,pa kutokea sioni,
Pande zote natazama,mkombozi simuoni,
Ndugu zangu wanisema,msaada siuoni,
Siku zangu nazipima,walimwengu kwaherini.


Nahara na kutapika,mwili wote ni vidonda,
Nywele nazo zanyonyoka,natisha nilivyokonda,
Mwili wote unanuka,mauti siwezi shinda,
Saa yangu imefika,najuta niliyotenda.


Ni wengi watafuata,nakiri nilisambaza,
Wengine wameshapita,wengine wazidi cheza,
Wasomi niliwachota,fukara sikubakiza,
Kweli leo ninajuta,nsamehe Mola muweza.


Jamaa wamenitenga,ndugu waninyanyapaa,
Mawazo yananisonga,kutengwa kunaniua,
Lini kusema ntafunga,wote siku wangojea,
Maji yashazidi unga,mauti yanyemelea.


Kwa macho hutamuona,unene sio kigezo,
Vijana mliopona,hima acheni mchezo,
Gonjwa lipo kila kona,acheni vitu vya dezo,
Nakufa bado kijana,kwa Mungu mimi chukizo.

Friday, September 11, 2009

Jua ni la utosini.

Asubuhi kunakucha,na njia ninaishika,
Ninapokwenda naficha,'tasema ntakapofika,
Nitapata ya mchicha?,swali liso na hakika,
Jua ni la utosini,linachoma si utani.


Ni wangu tena ujio,fungua pesa upate,
Chanuo na mafagio,ina njoo nikupake,
Anjifu na mitandio,mikufu pia na pete,
Jua ni la utosini,linachoma si utani.


Huruma siku yapita, ndururu sijainusa,
Watoto mimi najuta,viumbe waso na kosa,
Mitaa ninaipita,wateja spati kabisa,
Jua linanifuata,katu halitaki susa,
Jua ni la utosini,linachoma si utani.


Machinga ndo kazi yangu,mtaa hadi mtaa,
Kazi yanipa machungu,ila sikati tamaa,
Nachoka haki ya Mungu,umande nilikimbia.
Jua ni la utosini,linachoma si utani.


Mlo bahati someni, mwenzenu nilichezea,
Chenga nyingi shuleni,vitabu sikushangaa,
wasomi mataikuni,tuso skuli twaduwaa.
Jua ni la utosini,linachoma si utani.


Siombee umachinga,miguu yote yauma,
Bora jela kutinga,jua la utosi noma,
Pesa haujaichanga,fasta jua lishazama.
Jua ni la utosini,linachoma si utani.

Saturday, September 5, 2009

Wosia wa Babu

Wajukuu sikizeni,muda wangu umekwisha.
Leo nimewaiteni, muhimu kuwasilisha.
Sikiliza kwa makini,wala sitaki wachosha.


Mkamateni elimu,msimwache aendeze.
Hii ni nguzo muhimu,ili maisha uweze.
Hili ni langu jukumu,nawasihi muutunze.

Cha mwenzako si cha kwako,hilo sharti mlijue.
Tumia akili yako,muulize kapataje.
Kuiba na iwe mwiko,kwa jasho jitafutie.


Kweli kuweni makini,gonjwa lipo mtaani.
vya dezo kataeni,misaada tambueni.
'Siishi kwa tumaini,hasara tele nyumbani.

Maisha si lelemama,juhudi inawapasa.
Msikubali kukwama,sekunde hata lisaa.
Pande zote na tazama,pa kuanza hutokosa.

Kueni wavumilivu,matatizo yakabili.
Katu msiwe wavivu,msibaki na kandili.
Msile ulo mkavu,tulia penye kivuli.

Nguvu zinaniishia,nilosema yashikeni,
Huu ndo wangu wosia,ushikeni akilini.
Dunia itawambia,pembueni kwa makini.

Friday, July 31, 2009

Dini zetu ni kikwazo.

Mola nakupa heshima,ulimwengu uliumba.
leo mimi natazama,wapo waloshayafumba.
Kisa wazi nakisema,mimi na wangu mchumba.
dini zetu ni kikwazo,e Mola tusaidie.


Sio siri nampenda,shairi nimeandika.
kwa mwingine sitoenda,mistari niliishuka.
vishawishi nitashinda,nilisema na hakika.
dini zetu ni kikwazo, e mola tusaidie.


Mapenzi hayana dini,kabila wala hayana.
semi hizi kulikoni,hatarini kuachana.
ya kweli yangu imani,kamwe siwezi ikana.
Mwenzangu yake imani,msimamo kesha weka.
dini zetu ni kikwazo, e Mola tusaidie.


Wazaziwe wamfunza,kiburi wamjazia.
dini yake kuitunza,msimamo wamwekea.
wazaziwe wanibeza,kifupi wanichukia.
dini zetu ni kikwazo, e Mola tusaidie.


Baba mama walionya,kupenda kuliniteka.
Tayari walishaona,uzoefu 'litumika.
yakwao sikuyaona,kupenda kulifunika.
Dini zetu ni kikwazo, e Mola tusaidie.


Mwanangu hebu tulia,wa diniyo tampata.
chunga kutokujutia,matatizo tayapata.
haya nayakumbukia,rafiki alinisuta.
dini zetu ni kikwazo, e Mola tusaidie.


Njia panda bado nipo,sina pa kuelekea.
Nipeni njia mkato,mapenzi nayajutia.
Hima popote ulipo,ushauriwo "tapokea.

Friday, July 24, 2009

Sio siri nakupenda.

Miaka ilishapita,magumu niliyavuka.
Visiki nilivipita,wa maisha kumsaka.
Nilijua 'tampata,papara sikuzitaka.
Sio siri nakupenda,kwa mwingine sitoenda.


Natamani uwe wangu,niambie nitulie.
Ilikuwa siri yangu,imebidi nikujuze.
Niwambie ndugu zangu,baraka watujalie.
Sio siri nakupenda, kwa mwingine sitoenda.


Usiku hata mchana,nakuwaza nisikie.
Mapenzi yalomapana,nipokee unifiche.
Sio leo wala jana,penzi langu litambue.
Sio siri nakupenda,kwa mwingine sitoenda.


Sina sababu kupenda, ulivyo waniridhisha.
Sitake mimi kukonda,wewe ndo yangu maisha.
Naapa sitokutenda,hima sitobabaisha.
sio siri nakupenda, kwa mwingine sitoenda.


Tamati nimeifika,nambie unachowaza.
Kwako nimefika,sijui kama wakwanza.
Wewe utachotamka,moyoni tanituliza.
Sio siri nakupenda, kwa mwingine sitoenda.

Thursday, July 16, 2009

YATIMA JAMA HURUMA.

Yatima waso hatia,huruma napowakuta.
mlo wajitafutia,si hakika kuupata.
jalalani kuchokona,chochote watachopata.
yatima jama huruma,sio lao kusudio.


Magonjwa yawaandama,hakuna wa kuwatibu.
nani wa kuwatazama,maradhi yawaadhibu.
na chawa wawaandama,malazi yaso adabu.
yatima jama huruma,sio lao kusudio.


Mikononi mwa polisi,mkong'oto kama kazi.
maisha ya wasiwasi,watumiwa kwenye wizi.
zawakosa na risasi, kifo kipo waziwazi.
yatima jama huruma,sio lao kusudio.


Wengine pia hubakwa,ukimwi rahisi kupata.
Wengine hulawitiwa,makubwa na huwakuta.
miili yao yauzwa,
wengine kunufaika.
Yatima jama huruma, sio lao kusudio.


Wazazi nisikieni,tulieni msiruke,
ukimwi upo jamani,chunga usiwamalize.
malezi ni ya wazazi, walimwengu wako bize.
yatima jama huruma, sio lao kusudio.


Vijana siwasahau,kila jambo na wakati.
katu usijisahau,kuzaa kabla wakati.
wala usijejaribu,ngono siipe nafasi.
yatima jama huruma,sio lao kusudio.


Yapo mengi yawasibu,siwezi yote eleza.
Sote na tunawajibu,kutoa tunachoweza.
Elimu kwao muhimu,hamasika kuwatunza.
Yatima jama huruma, sio lao kusudio.

Tuesday, July 14, 2009

NINI WAMETUFANYIA?

Uchaguzi mbili kumi,huo hapo wajongea.
Waja kuisaka kumi, wako waliolowea.
wametufanyia nini, jibu sharti kutupatia.
tuamke wajameni,tuchague wa kutusaidia.
Kura fika haki yako,umpendaye mchague.
hupotezi muda wako,uhakika wa badae.
nini wametufanyia,waulizwe bila woga.

Tarehe itawadia,kampeni kuzipiga.
Waongo utawajua,'tazijua zao soga.
uwezo kuzingatia, zawadi wakizimwaga.
nini wametufanyia,waulizwe bila woga.


Takrima usikubali,mzalendo 'ndo kigezo.
yule atayekujali, hela isiwe kigezo.
Usiukubali wali,wala tisheti za dezo.
nini wametufanyia,waulize bila woga.


Wageni watatujia,yakwao watatwambia.
nini watatufanyia,bayana kutuwekea.
zipi 'takuwa hatua,wasipotutimizia?
nini wametufanyia,waulizwe bila woga.

Kalamu naweka chini,jamani tuwe makini.
somo lipo akilini,mitano hiyo ni mingi.
nne moja fomesheni,kamchezo kasomeni.
nini wamefanya,waulizwe bila woga.