Monday, March 29, 2010

Nakutafuta amani.

Ajali kila uchao,maisha yanapotea,
wapo wengi hatunao,kwa mola wametangulia,
viongozi soni kwao,lawama twawatupia,
Nakutafuta amani,waongewa sikuoni.

Rushwa iliyokithiri,masikini waonewa,
wakubwa wanakiburi,uchumi wahujumiwa,
pesa kitu jeuri,sheria yapinduliwa,
Nakutafuta amani,waongewa sikuoni.

Ufisadi wabobea,wahusika wanafichwa,
serikali inawajua,majina wanatunziwa,
chamani waogelea,uswahiba twaelewa,
Nakutafuta amani,waongewa sikuoni.

Maji ni kubwa tatizo,watu wanahangaika,
umbali sio mchezo,kina mama wanachoka,
umeme bado gumzo,ni lini taimarika,
Nakutafuta amani,waongewa sikuoni.

Elimu iliyo duni,watoto wataabika,
wanakaa mavumbini,kwa shida wanaandika,
viongozi amkeni,kuonewa tumechoka,
Nakutafuta amani,waongewa sikuoni.

Maisha yaliyo bora,maneno yatamkika,
walitaka hizo kura,kapuni wakatuweka,
twaishi kama chokora,na siku zinakatika,
Nakutafuta amani,waongewa sikuoni.

Hii Tanzania yangu,yenye wingi wa maneno,
amani hili ni jungu,lakwaza si mfano,
amani wapi wandugu,latumika ka'ndoano,
Nakutafuta amani,waongewa sikuoni.