Monday, October 4, 2010

Joka mbona huzeeki?

Upo toka Tanganyika, hadi sasa Tanzania,
Msingi aliuweka, baba kesha tangulia,
Tayari tungeshafika, Nyerere angendelea,
Joka mbona huzeeki, binafsi nimekuchoka.

Chumvi yote ulokula, tumia basi busara,
Ifike tena pahala, hima iamue kura,
Watu ndio wenye hila, chombo hakina papara,
Joka mbona huzeeki, binafsi nimekuchoka.

Wajengao hicho chombo, kizalendo watafteni,
Ndani kimejaa shombo, chaoshwa kwenye kampeni,
Waambulia kikumbo, watetezi wa maskini,
Joka mbona huzeeki, binafsi nimekuchoka.

Kalamu ninaiacha,wino kamwe hutokwisha,
Joka ondoa makucha, malengo kufanikisha,
Tazama panavyokucha, huna budi kutupisha,
Joka mbona huzeeki, binafsi nimekuchoka.

Uzee busara bwana, zeeka inakubidi,
Kwanini unang'ang'ana , twajua ushafaidi,
Wapeni nao vijana, tuifikie ahadi,
Joka mbona huzeeki, binafsi nimekuchoka.