Friday, December 23, 2011

Laiti angekuwepo

Kauli i'lozagaa, ya tamaa kuikata,
U wapi u'lotufaa, twatamani kukufwata,
Nchi inachechemea, ni mengi yanatukuta,
Laiti angekuwepo, mbona Kingunge tunaye?

Ngombale bado tunaye, hima tumtumieni,
Nyerere hatupo naye, fikra'ze zipo vichwani,
Busara'ze ajuaye, Kingunge hoja mezani.
Laiti angekuwepo, Mama Nyerere tunaye.

Mama yetu wa Taifa, ana mengi kutufunza,
Laiti hii ni kashfa, mama bado anaweza,
Kujuta wala si sifa, busara'ze si kubeza,
Laiti angekuwepo, Malecela mbona yupo?

Tokea enzi za baba, alikuwapo Msuya,
Busara alizishiba, wala takrima hakula,
Mbinu bado kazibeba, atumiwe bila hila,
Laiti angekuwepo, mbona wengi bado wapo?

Hebu tuwape nafasi, historia wapakue,
Makovu yake nanasi, utamu'we palepale,
Tuache mawazo hasi, wazee wasaidie,
Laiti angekuwepo, wapo tuwatumieni.

Laiti si neno zuri, twende mbele Tanzania,
Uzalendo ndio siri, tujibidishe kwa nia,
Bila Nyerere si shwari, msemo wa mazoea,
Laiti angekuwepo, mawazoye twatumia?

Wapo wengi wa zamani, enzi zile za Mwalimu,
Ni wachache shairini, wote kuwepo ni ngumu,
Tupeni dira jamani, wa mwalimu mu muhimu,
Laiti angekuwepo, Mpo wengi m'lo tunu.