Friday, May 20, 2011

Ajali zaepukika!

Jamani nisikizeni, nisomeni waungwana,
Nafichani moyoni, lipi lisojulikana,
Ajali tele pomoni, usiku hata mchana,
Madereva mwahusika, ajali zaepukika.

Wa mabasi wamiliki, amueni mtaweza,
Andaeni mikakati, ajali kutokomeza,
Magari muyahakiki, kabla safari kuanza.
Madereva yao haki, wapeni bila kupinda.

Ulevi na muuache, madereva mwahusika.
Subiri hima kukuche, usiku hamtafika.
Sheria mzitumie, mnazitambua fika.
Madereva mtulie, ajali zaepukika.

Ajali zimekithiri, za mabasi si kificho,
Vita si ya hiari, fungueni yenu macho,
Maisha ya wasafiri, bora ya mboni ya jicho,
Kukumbushwa msisubiri, ajali zaepukika.

Abiria kataeni, mwendo uliomkali,
Roho zenu teteeni, si budi kuwa wakali,
Mikanda katika siti, fungeni kwa kila hali.
Wasafiri unganeni, uhai wenu chungeni.

Polisi barabarani, mwahusika siwafichi,
Rushwa sasa acheni, wateteeni wananchi,
Magari ya'lo walakini, hakikisha huyaachi.
Usalama dumisheni, ajali 'taepukika.

Wasanii Five Star, walipoteza maisha,
Ajali twakumbukia, uzembe lisababisha,
Mv bukoba nakumbushia, uzembe umetutosha,
Meli ilielemea, ukweli sitopindisha.

Amani umetutoka, Kessy tulikuhitaji,
Tunalia tunachoka, ajali "mekuwa jaji,
Ajalini 'mekufika, mauti yasotaraji,
Ajali 'metunyang'anya, rafiki yetu mkubwa.

Abiria ushikeni, huu wangu ushauri,
Kulala na epukeni, pindi mnapo safiri,
Magazetini kunani, iwe mwisho wa safari.
Hakuna jipya fanani, yote nayakariri.

Sina tena la ziada, zinaepukika ajali,
Hebu hii iwe mada, namna ya kukabili,
Uhai vema kulinda, tena kwa hali na mali.
Janga si la kawaida, tujipange kukabili.