Sunday, December 20, 2009

Waridi.

Ua ninakutafuta, tayari ushachanua,
Marashi nanayapata,manukato yavutia,
Ni lini nitakupata,uzuri najivunia,
Waridi nakutafuta, nataka kujichumia.


Niite unionapo, wala usibabaike,
Sijui wapi ulipo,paza sauti iskike,
Ipi ni njia mkato, haraka mimi nifike,
Waridi nakutafuta, nataka kujichumia.


Ni mengi ninayaona, maua ya kupendeza,
Ni lipi lililonona,si kazi ya kubeza,
Waridi ndo lanikuna,ua litaniliwaza,
Waridi nakutafuta, nataka kujichumia.

Waridi ninakusaka,wa maisha jitokeze,
Mbali pia nitafika,ulipo wewe nijuze,
ua umeshapevuka,nakuchuma nikutunze,
Waridi nakutafuta, nataka kujichumia.

Bustanini ninapita,tayari kujichumia,
Tabia itanivuta,ua kufuatilia,
Najua nitalipata,maisha tafurahia.
Waridi nakutafuta, nataka kujichumia.