Friday, October 9, 2009

Maisha

Maisha kweli ni fumbo,lilogumu kufumbua,
Leo lakupiga kumbo,kesho wachekelea,
Punde yezaenda kombo,sharti kujikwamua,
Maisha ndivyo yalivyo,ya kesho huwezi jua.


Maisha yamesheheni,uzuri pia ubaya,
Ungalipo duniani,usiyaonee haya,
Popote yatafuteni,msichoke kusakanya,
Maisha ndivyo yalivyo,ya kesho huwezi jua.


Usitukane wakunga,na uzazi bado upo,
Mlango utafunga,ungali ndani haupo,
Meli maisha tasonga,taachwa hapo ulipo.
Maisha ndivyo yalivyo,ya kesho huwezi jua.


Njiani utayakuta,majabali vizingiti,
Huna budi kuyapita,viunzi havikwepeki,
Kamwe hakuna kujuta,maisha nasbu bahati,
Maisha ndivyo yalivyo,ya kesho huwezi jua.